Mashabulizi dhidi ya raia yakomeshwe mara moja-Yamamoto
Watu takriban 15 wameuawa na wengine 40 wamejeruhiwa katika shambulio nchini Afghanistan.
Shambulio hilo limetokea Lashkargah, mji mkuu wa jimbo la Helmand nchini Afghanistan.
Akilaani shambulio hilo, na kutaka mashambulizi kama hayo kukomeshwa mara moja, mwakilishi malum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa nchini Afghanistan, Tadamichi Yamamoto, amesema kuwa shambulio dhidi ya raia waliokuwa wanatoka michezoni ni kinyume na maadili na kutaka vitendo kama hivyo kukomeshwa mara moja
Ameongeza kuwa wakati huu ambapo raia wa nchi hiyo wanasubiria amani, visa kama hivyo visivunje nguvu azma yao ya kutafuta juhudi za pamoja za kumaliza mgogoro huo.
Shambulio hilo lilitokana na kulipuliwa kwa lori moja lililokuwa limejaa vilipuzi ambalo lilikuwa limeegeshwa karibu na eneo la maegesho ya magari.
Yamamoto ambaye pia ni mkuu wa uJumbe wa Umoja wa Mataifa nchini Afghanistan UNAMA amesema kuwa hakuna sababu yoyote inayoweza kutolewa kuhalalisha shambulio hilo,linaloweza kuwa kosa la uhalifu wa kivita na kutaka waliohusika wachukuliwe hatua za kisheria na kuwajibishwa.
Yamamoto, ametoa rambirambi zake kwa familia za waliouawa katika shambulio hilo pamoja na kuwatakia ahueni majeruhi.