Ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu unaendelea Uturuki: Zeid
Ripoti ya ofisi ya haki za binadamu ya Umoja wa Mataifa imebaini kwamba hali ya dharura iliyotangazwa kwa mfululizo na mamlaka nchini Uturuki imesababisha ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu dhidi ya maelfu ya raia nchini humo.
Kwa mujibu wa ripoti hiyo inayojumuisha matukio ya tarehe mosi Januari hadi Disemba 2017, baada ya jaribio la kumpindua rais Recep Tayyip Erdoğan hapo tarehe 15 Julai mwaka 2016, imesababisha ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu, mmomonyoko wa utawala wa sheria nchini Uturuki, na huenda ikaathiri hali ya kiuchumi siku za usoni.
Bwana Zeid Ra’ad Al Hussein mkuu wa ofisi ya haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa amesema hadi sasa zaidi ya watu 160,000 wametiwa nguvuni , watumishi wa umma laki moja na nusu ikiwemo, walimu, majaji na wanasheria wamefukuzwa kazi ndani ya miezi 18 tu, huku zaidi ya waandishi wa wahabari 300 na wanaharati wa haki za binadamu kutiwa mbaroni bila kufuata taratibu za kisheria kwa mujibu wa sheria ya kimataifa.
Ripoti hiyo imekusanywa kutokana na ushahidi wa ndugu wa wahanga waliofanikiwa kutoroka ,uchambuzi wa habari za Serikali, nyaraka za vyanzo huru , picha za satelaiti na pia vyanzo vingine vinavyoaminika .
Ofisi ya haki za binadamu imetoa wito kwa serikali ya Uturuki kuruhusu Ofisi ya haki za binadamu kufanya uchunguzi kamili, kufanya kazi kwa uhuru na kwa kujitegemea ili iweze kufanya tathmini sahihi ya hali ya haki za binadamu Kusini-Mashariki mwa nchi hiyo.