Wakimbizi wa DRC waendelea kumiminika Uganda: UNHCR
Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi , UNHCR leo linasema wakimbizi kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo-DRC- wanaoingia Uganda, wanaongezeka kila uchao kwa kiwango kisicho cha kawaida.
UNHCR inasema wakimbizi hao ambao asilimia kubwa ni wanawake na watoto wanatokea maeneo ya Mashariki mwa DRC . Kama anavyofafanua msemaji wa UNHCR, Babar Baloch mbele ya waandishi habari mjini Geneva, Uswisi wakimbizi hao wanatoroka mapigano mabaya ya kikabila na pia vitendo vya unyanyasaji wa kingono vinavyoendelea nchini mwao.
(SAUTI YA BABAR)
“Katika kipindi cha siku tatu, kati ya tarehe 10 hadi 13 Machi, zaidi ya watu 4,000 walivuka mpaka na kuingia Uganda kutoka mikoa ya Ituiri,na Kivu kaskazini. Idadi hii ni kubwa ikilinganishwa na mwaka 2017 wakati takriban watu 44,000 walikimbilia machafuko kwa kipindi cha mwaka mzima.”
Ameongeza kuwa UNHCR inahofu kuwa huenda maelfu zaidi wanaweza kuwasili Uganda ikiwa hali ya kiusalama ndani ya DRC haitotengamaa haraka.
Wakimbizi hao wanaoingia Uganda kutoka Ituri wanatumia mitumbwi ambayo ni hatari kwa usalama wao kuvuka ziwa Albert safari ambayo imesababisha baadhi ya wakimbizi kupoteza maisha yao.