Usawa wa kijinsia ndio mkatakati wangu-Guterres

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres amesema kuwa uongozi wake unatilia mkazo usawa wa kijinsia katika ngazi zote uongozi katika shirika hilo.
Katibu Mkuu ameyasema hayo leo mjini New York, Marekani wakati anakutana na wawakilishi wa mashirika ya kiraia, pembezoni mwa mkutano wa 62 wa kamisheni ya hali ya wanawake dunaini, CSW62.
Ametoa mfano wa mgawanyo wa kijinsia katika menejimenti ya juu kabisa ya Umoja wa Mataifa akisema alipochukua hatamu wanaume walikuwa asilimia 60 ilhali wanawake asilimia 40 na kueleza hali ilivyo kwa sasa.
(Sauti ya Antonio Guterres)
“Sasa, badala ya asilimia 60 ya wanaume na asilimia 40 ya wanawake tuna asilimia 56 ya wanawake asilimia 44 ya wanaume.”
Pia amesema kuwa shabaha yake nyingine kuu ni kupiga vita vitendo vya unyanyasaji wa kingono vilivyoripotiwa kufanywa na watendaji wa mshirika ya Umoja wa Mataifa dhidi ya watu wa nje.
(Sauti ya Antonio Guterres)
“Hii ni shida iliyoko katika vikosi vya kulinda amani na pia katika mashirika mengine ya utoaji misaada huko mashinani”
Hata hivyo Bwana Guterres amesema wanafanya kila liwezekanalo kuweza kuondoa tatizo hilo akisema japo sera ya kutovumilia visa hivyo ilitangazwa muda mrefu uliopita bado tatizo ni utekelezaji.