Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

IOM itasimama kidete na wanawake wahamiaji popote walipo

Wanawake duniani kote tushikamane!
UN Women
Wanawake duniani kote tushikamane!

IOM itasimama kidete na wanawake wahamiaji popote walipo

Wanawake

Ikiwa leo  ni maadhimisho ya siku ya wanawake dunia, Shirika la Umoja wa Mataifa la uhamiaji IOM, limesema litasimama kidete  kumtetea na kumlinda kila mwanamke au msichana mhamiaji mwenye moyo wenye  wa matumaini, akili iliyojaa mawazo ya maendeleo popote alipo duniani.

Mkurugenzi wa IOM Wiliam Lacy Swing katika ujumbe wake siku ya wanawake yenye kaulimbiu “wakati ni sasa” amesema, bila kujali rika, kabila, rangi na hali ya kiuchumi, IOM  pamoja na Umoja wa Mataifa  wako bega kwa bega kuhakikisha kila mwanamke na msichana anaalindwa na kuwezeshwa katika dunia hii iliyojaa mfumo dume wanayokabiliana nao.

Halikadhalika bwana Swing amesema uwezeshwaji wa wanawake ni mwanzo kuinua jamii yote  kwa ujumla, hivyo IOM inashirikiana na mamlaka zote za uhamiaji kuzuia na kupambana na aina zote za unyanyasaji na ubaguzi dhidi ya wanawake na wasichana, na kushughulikia masuala mbalimbali ya kimuundo ambayo husababisha unyanyasaji huu na ubaguzi.

Ameongeza kuwa katika mazingira ya uhamiaji mwanamke ndie anaekabiliwa na majukumu makubwa ya kulinda  na kuiwezesha jamii, katika kutafuta kazi, kulea watoto, na majukumu ya kifamilia mengine muhimu kuliko wanaume.

Katika maadhimisho ya leo IOM inasimama na wanawake wote katika  heshima maalum kwa washirika wanaojitahidi kutetea haki za wanawake na wasichana. IOM itaendelea kusimama na wanawake wahamiaji kila uchao katika kuhakikisha haki inatendeka bila kujali hali zao.