Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Watu zaidi ya 40 kuwajibishwa kwa uhalifu wa vita na dhidi ya ubinadamu Sudan kusini

UN Photo/Isaac Billy
Bi Yasmin Sooka mwenyekiti wa tume ya haki za binadamu ya Umoja wa mataifa Sudan Kusini akizungumza na waandishi wa habari. Picha:

Watu zaidi ya 40 kuwajibishwa kwa uhalifu wa vita na dhidi ya ubinadamu Sudan kusini

Amani na Usalama

Tume ya haki za binadamu ya Umoja wa Mataifa inakusanya ushahidi ili kuwawajibisha maafisa wa Sudan kusini zaidi ya 40 kwa makosa ya uhalifu wa kivita na uhalifu dhidi ya ubinadamu.

Kwa mujibu wa ripoti iliyotolewa leo na tume hiyo ya haki za binadamu Sudan Kusini, ambayo ni ripoti ya kwanza tangu ilipopewa jukumu la kukusanya na kuwasilisha ushahidi utakaotumika kwenye mahakama ya uhalifu na njia zingine za uwajibikaji zilizoafikiwa chini ya mkataba wa amani wa 2015, imesema imebaini maafisa zaidi ya 40 wa jeshi ambao watabeba majukumu binafsi ya uhalifu huo.

Yasmin Sooka ambaye ni mwenyekiti wa tume hiyo amesema “Chini ya mkataba wa amani, watakaofunguliwa mashitaka hawawezi tena kushikilia au kugombea wadhifa wowote. Hatimaye hii ndiyo njia pekee ya kukomesha uharibifu wa maisha ya mamilioni ya watu unaofanywa na viongozi wa Sudan kusini.”

Ripoti hiyo inaainisha ukatili wa hali ya juu dhidi ya raia ikiwemo macho yao kunyofolewa, kukatwa makoromeo au kuhasiwa, watu kubakwa akiwemo ajuza wa miaka 85 aliyebakwa na genge la watu na kisha kushuhudia mwanae na mumewe wakiuawa kikatili,  pia watoto kuingizwa jeshini na pande zote katika mzozo huku wakishinikizwa kuua raia. Mjumbe wa tume hiyo Andrew Clapham ameongeza

(SAUTI YA ANDREW CLAPHAM)

“ Mapendezo ya msingi katika ripoti yetu ni kwamba mahakama ya mseto ambayo serikali ya Sudan kusni na AU wameiafiki ni lazima ianzishwe mara moja na mwendesha mashitaka aanze kuandaa kesi sio dhiti tu ya wale waliohusika moja kwa moja pia wale waliokuwa katika malaka ya kutoa amri, waliojua nini kinaendelea na wakashindwa kuchukua hatua.”