Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ajira milioni 12 zahitajika kila mwaka Afrika kunusuru vijana:FAO

Ukosefu wa ajira ni mwiba zaidi kwa vijana. (Picha:UN/ILO)

Ajira milioni 12 zahitajika kila mwaka Afrika kunusuru vijana:FAO

Sekta ya kilimo ni tegemeo la ajira kwa vijana barani Afrika, hivyo ni vyema kuchukua hatua ili kilimo kiwe cha tija.

Kila mwaka barani Afrika ajira milioni 12 zinahitajika ili kukidhi mahitaji ya vijana wanaoingia katika soko la ajira kwa kipindi cha miaka 20 ijayo. Selina Jerobon na taarifa kamili.

(Taarifa ya Selina Jerobon)

Hayo yameelezwa leo kwenye mkutano wa 30 wa shirika la chakula na kilimo FAO kwa ajili ya kanda ya Afrika unaofanyika mjini Khartoum Sudan ,ukijikita katika mada ya “kuunda ajira zenye hadhi na za kuvutia barani humo hususani kwa vijana.”

Akizungumza katika mkutano huo mkurugenzi mkuu wa FAO José Graziano da Silva amesema kilimo kitaendelea kuwa uti wa mgongo na muajiri mkubwa barani Afrika katika miongo ijayo lakini fursa mpya zisakwe zitakazokuwa zaidi ya kilimo  katika mfumo mzima wa chakula ili kuunda ajira za kutosha kwa vijana hususani walioko vijijini.

Ameongeza kuwa leo hii asilimia 54 ya nguvu kazi barani Afrika inategemea sekta ya kilimo kwa maisha ya kila siku, kipato na ajira, na kwa idadi kubwa ya watu kuhamia mijini mahitaji ya soko la chakula yanakuwa, hali ambayo inaweza kutoa fursa za ajira katika shughuli zote zinazohusiana na kilimo.

Tony Nsanganira ni mtaalamu wa programu ya ajira ya vijana wa FAO kwa ajili ya kanda ya Afrika na anasisitiza

( Sauti ya Tony Nsanganira)

“Ni muhimu sana kuendelea kuangali fursa za kuwahakikishia vijana ajira ili kuepuka hatua ya kuhama , lakini pia tunatambua kwamba vijana kuwa ndio kundi kubwa katika jamii watachangia katika kuleta mabadiliko kwenye bara hili na hususani vijijini.”

 Ameongeza kuwa nchi zinapaswa kuchagiza mabadiliko vijijini na kujenga madaraja baina ya shughuli za kilimo na nyinginezo , vijijini na mijini na katika nyanja mbaimbali ikiwemo uandaaji, usindikaji, ufungaji, usafirishaji, usambazaji, masoko na utoaji huduma zikiwemo za kifedha na kibiashara.