Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Madai mengine ya unyanyasaji wa kingono yaibuka MONUSCO DRC

Msemaji wa Umoja wa Mataifa Stephane Dujarric akizungumza na waandishi wa habari wakati akitangaza tamko la UM kufuatia hatua ya Marekani. (Picha:VideoCapture)

Madai mengine ya unyanyasaji wa kingono yaibuka MONUSCO DRC

Amani na Usalama

Msemaji wa katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Stephane Dujarric amesema ofisi ya mpango wa Umoja wa Mataifa nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC-(MONUSCO) imepokea madai mengine ya miendendo mibaya ikiwemo unyanyasaji wa kingono, ukiwahusisha walinda amani kutoka Afrika Kusini.

Akizungumza na waandishi habari mjini New York, Durarric amesema taarifa mpya  zaonyesha kuna madai matatu ya unyanyasaji wa kingono yaliyohusisha watu kadhaa.

Sauti ya Stephane Dujarric 

“Kwa mujibu wa taarifa  tulizonazo, madai matatu ya unyanyasaji wa kingono ukiwahusisha watu wazima watatu, moja likiwa la kuwa baba na lingine kuhusu madai ya matunzo kwa mtoto. Inadaiwa matukio hayo yalifanyika  sehemu za sake, Beni na Goma katika mkoa wa Kivu Kaskazini. Shirika la UNFPA limekuwa likihusika ili kuhakikisha kuwa waathiriwa wanapata msaada wa haraka”..

Nalo dai la nne linahusu mvulana wa miaka 17 kupigwa na mlinda amani Mashariki mwa Kasai. Muathirika ameelekezwa kwa UNICEF ili kupata msaada na ulinzi na anachunguzwa na  ofisi ya pamoja na haki za binadamu.

Stephane ameongeza kuwa  Umoja wa Mataifa tayari umeifahamisha serikali ya Afrika Kusini kuhusu madai hayo.

sauti ya Stephane Durarric

Umoja wa Mataifa umeshaiarifu nchi ya watu husika na kuiomba  iteue maafisa  wakitaifa wa uchunguzuzi katika kipindi cha siku tano na kuwa uchunguzi wa Madai hayo ukamilishwe chini ya mda wa siku 90, na kwamba uchunguzi huo utafanyika kwa pamoja na  timu kutoka ofisi ya huduma za masuala ya ndani.”

Dujarric amesisitiza kuwa  mkakati wa Umoja wa Mataifa  ni kuhakikisha kuwa waathirika wanapata msaada na pia MONUSCO itachangia  msaada kama vile kukusanya sampuli za viini nasaba-DNA na kusikitishwa na madai ya unyanyasaji wa kingono licha ya  juhudi kwa nchi  washirika  za kuzuia na kushughulikia  unyanyasaji wa kingono.