Mapigano CAR yasababisha maelfu kukimbilia Chad
Huko nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati, CAR, ghasia mpya zilizozuka nchini humo zimefurusha maelfu ya watu ambao sasa wameingia nchini Chad. Selina Jerobon na ripoti kamili.
(Taarifa ya Selina Jerobon)
Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudmia wakimbizi, UNHCR, limesema ghasia hizo zinatokana na mapigano kati ya vikundi vilivyojihami kwenye mji wa Paoua katika jimbo la kaskazini magharibi la Ouam-Pende.
Vikundi hivyo ni kile cha ukombozi wa CAR, MNLC na kile cha mapinduzi na haki, RJ ambapo zaidi ya wakimbizi 2300 wameingia kusini mwa Chad.
UNHCR inasema idadi hiyo ni kubwa ikilinganishwa na wakimbizi 2000 walioingia mwaka jana nchini Chad kutoka CAR.
Wakimbzi hao wanaripoti kukabiliwa na vitendo vya ukiukwaji wa haki kutoka vikundi hivyo vilivyojihami.
Ingawa mpaka kati ya CAR na Chad umefungwa, mamlama za Chad zinatumia ubinadamu kuachia wakimbizi kuingia nchini mwake, jambo lilipongezwa na UNHCR.
Nao Umoja wa Mataifa kupitia naibu msemaji wake, Farhan Haq umezungumzia masikitiko yake juu ya kinachoendelea huko CAR hususan ugumu unaosababishwa na vikundi vilivyojihami..
(Sauti ya Farhan Haq)
“Uwepo wa vikundi hivyo ulivyojihami mjini humo unakwamisha hali kurejea katika hali ya kawaida. Ujumbe wa Umoja wa Mataifa nchini humo unaimarisha vikosi vyake pamoja na doria ili kuepusha mashambulizi dhidi ya raia.”