Vijana tumieni mitandao ya kijamii kujiendeleza
Nchini Afghanistan, vijana wametakiwa kutumia fursa ya mitandao ya kijamii ili kujikwamua kimaendeleo. Assumpta Massoi na ripoti kamili.
(Taarifa ya Assumpta Massoi)
Vijana wa Kike na wa kiume nchini Afghanistani walikutana kwa siku tano huko Herat ambako lengo kubwa lilikuwa kuwahamasisha juu ya kujiendeleza na kuepuka vitendo vya kigaidi.
Baraza la mashauriano la vijana linaloangazia masuala ya maendeleo, vita dhidi ya vitendo vya kigaidi na pia hamasa kwa vijana nchini Afghanistan liliandaa jukwaa hilo la vijana kwa udau na ujumbe wa Umoja wa Mataifa nchini Afghanistan, UNAMA.
Vijana walichangia mawazo mbalimbali ikiwemo mikakati ya kupiga vita itikadi za kigaidi na fursa za ajira kwa vijana ambao ni waathirka wakubwa wa ajira nchini Afghanistan.
Bwana Tawab Mobarez, ambaye ni mratibu wa kitengo cha vijana kwenye serikali ya jimbo la Herat na pia msemaji mkuu katika kongamano hilo alisema baada ya kuzungumza na vijana wengi, ni dhahiri kwamba swala la amani, usalama , na pia vita dhidi ya itikadi ya kigaidi kwa vijana ni suala mtambuka ambalo litawanusuru vijana katika fikra potofu na za kimasikini.
Pia alishukuru jitihada za UNAMA kuandaa kongamano hilo ambalo ni jitihada za kutambua umuhimu wa vijana nchini humo, ambao ndio msingi wa mustakabali wa uchumi wa nchi hiyo.
UNAMA imeendelea na mikakati ya kuwafikia vijana, wazee, wanawake nchini Afghanistan katika jitihada za kutafuta amani ya kudumu na pia maendeleo kwa jamii yote kwa ushirikiano na serikali na pia asasi za kiraia.