Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Utapia mlo wawazonga watoto Venezuela:UNICEF

Wanunusi wanapanga foleni masaa tano kununua mkate unaopimwa kiwango kidogo kwa kila mmoja kutoka kwa bakery ndogo huko Cumaná, Venezuela. Picha: Meridith Kohut / IRIN

Utapia mlo wawazonga watoto Venezuela:UNICEF

Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto la UNICEF limeonya kuwa  idadi kubwa ya watoto nchini Venezuela wanakabiliwa utapiamlo kutokana na athari za mgogoro wa kiuchumi unaolikumba taifa hilo.

Ingawa takwimu kamili hazipo kutokana na kutopatikana kwa data za lishe na za afya , kuna dalili tosha za kuwa mgororo huo unawazuia watoto kupata huduma  bora za afya, madawa pamoja na lishe.

Hali hiyo imelilazimisha shirika la UNICEF kutoa wito wa kutekeleza  mkakati wa dharura wa kukabiliana na utapiamlo kwa ushirikiano kati ya serikali na  wadau wake.

Takwimu rasmi na pekee zilizoko ni za mwaka 2009 ambazo zinaonyesha afya duni kutokana na ulinganifu wa uzito na urefu kwa watoto walio chini ya umri wa miaka mitano, wakati huo ulikuwa  asili mia 3.2. Hata hivyo takwimu mpya  na ambazo si rasmi, zimeonyesha kama idadi ya watoto wenye afya duni ni kubwa zaidi.

Nayo ripoti ya dunia ya lishe ya mwaka 2016 inakadiria kwamba kiwango cha afya duni miongoni mwa watoto ni  asilimia 4.1 huku ripoti ya taifa kuhusu chakula na lishe duniani ya mwaka 2017 ikisema kwamba kiwango cha lishe duni nchini Venezuela kimeongezeka.