Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Haki za wahamiaji ziheshimiwe:UN

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres akihutubia Baraza Kuu kuhusu uhamiaji 01.11.2018 (maktaba). Picha: UM/Mark Garten

Haki za wahamiaji ziheshimiwe:UN

Heshima pamoja na haki vya wahamiaji na wakimbizi , kwa mujibu wa  msemaji wa Umoja wa Mataifa, ni sharti viheshimiwe popote pale. Stéphane Dujarric amesema hayo Ijumaa akijibu maswali kuhusu matamshi yanayodaiwa kutolewa na rais wa Marekani Donald Trump akizishushia hadhi nchi za kiafrika pamoja na watu kutoka Haiti.

Hata hivyo Bwana Trump amekanusha madai ya kutumia lugha  mbaya kwenye mkutano katika Ikulu ya Marekani, White House, ingawa  wabunge kadhaa wa baraza la Senate la Marekani , wamenukuliwa na vyanzo mbalimbali vya habari Ijumaa waisema kuwa  maneno aliyotumia yalijawa na kile kilichoitwa,  chuki , aibu na ni ya kibaguzi.

Bwana Dujarric, alipoulizwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa anasemaji kuhusu madai ya matamshi hayo ya Rais Trump?,amewataka waandishi wa habari kutafakari hotuba ya Bwana Guterres, aliyoitoa Alhamisi wiki hii wakati, akitoa mwongozo wa ripoti yake mpya yenye kichwa cha maneno,  ‘ kufanya uhamiaji kuwafaa wote na kumnukuu akisema’.

(SAUTI YA STEPHANE DUJARRIC-MSEMAJI WA UN)

“Hadhi na haki za kibinadamu pamoja na usawa kwa wale wote wanaohama kutafuta maisha bora, vinahitaji kuheshimiwa popote pale.” 

Mapema leo Ijumaa msemaji wa  ofisi ya Umoja wa Mataifa ya haki za binadamu mjini Geneva Uswisi , Rupert Colville, alikuwa na haya ya kusema kuhusu suala hilo

(SAUTI YARUPERT COLVILLE-MSEMAJI WA OFISI YA HAKI ZA BINADAMU)

“ Endapo yatadhibitishwa,  haya ni matamshi yanayoshtua na yenye fedheha kufanywa na rais wa Marekani. Nasikitika lakini hakuna neno lingine la kutumiwa bali kuitwa ya kibaguzi. Hizi si taarifa kuhusu lugha chafu bali  kufungua mlango kuona upande mwingine mbaya wa mwanadamu. Hii ni kama kuhalalisha na kuhimiza ubaguzi  pamoja na chuki dhidi ya wageni jambo ambalo litavuruga na pia kuharibu maisha ya watu wengi.”