Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Hatimaye uwanja wa Ndege Puntland wafunguliwa: IOM

Dyane Epstein, Mkuu wa IOM Somalia wakati wa sherehe ya ufunguzi wa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Garowe nchini Somalia. Picha: (IOM) 2018

Hatimaye uwanja wa Ndege Puntland wafunguliwa: IOM

Ukarabati kwenye uwanja wa ndege wa kimataifa wa jimbo la Puntland- Somalia umekamilika kwa msaada wa shirika la Umoja wa Mataifa la uhamiaji IOM  na sasa umeanza tena kufanya kazi baada ya kufungwa  kwa kipindi cha miaka kumi na mitano iliopita. John Kibego  anatupa maelezo zaidi

(TAARIFA YA JOHN KIBEGO)

Uwanja huo unapatikana katika mji mkuu wa jimbo hilo -Garowe. Utawala wa Puntland ndio uliongoza shughuli za kuukarabati  huku shirika la uhamiaji la IOM likipiga jeki juhudi hizo kwa ushirikiano wa  serikali kuu ya Somalia pamoja na wadau wengine  wa kimataifa.

Katika sherehe ya ufunguzi wa uwanja huo mkuu wa shirika la IOM ofisi ya Somalia , Dyane Epstein, amesema, kuwepo kwa uwanja wa ndege unaofanya kazi barabara mjini Garowe ni mmoja ya hatua nzuri kuelekea mustakbala bora wa uhamiaji,kuwezesha kurahisisha shughuli za  kuingia na kutoka , sio tu katika jimbo la Puntland lakini pia Somalia nzima kwa ujumla.

Naye naibu waziri wa   masula ya safari za ndege pamoja na viwanja katika jimbo hilo, Suad Salah Nurm, ameupongeza ushirikiano uliopo kati ya serikali ya jimbo la Puntland, na serikali kuu ya Somalia pamoja na washirika wao wa kimataifa likiwemo shirika la IOM kwa kufanikisha juhudi za kurejesha upya kazi za uwanja huo wa ndege wa Garowe.

Miongoni mwa waliohudhuria sherehe hiyo iliofanyika wiki hii  ni pamoja na  vigogo kutoka serikali ya mkoa huo  akiwemo rais wa Somalia, Mohamed Abdullahi Farmajo. Wengine ni wajumbe kutoka Umoja wa Ulaya, Benki ya Dunia, Umoja wa Mataifa na vile vile kutoka serikali za Uturuki na Ethiopia.