IOM kushirikiana na UNICEF kuokoa watoto wahamiaji Libya
Shirika la Umoja wa Mataifa la uhamiaji IOM, limesema linashirikiana na mashirika mengine ya Umoja wa Mataifa kama UNICEF katika kutafuta ufumbuzi wa suala la wahamiaji hasa watoto wasio na walezi nchini Libya. John Kibego na maelezo zaidi.
(Taarifa ya John Kibego)
Othman Belbeisi ambaye ni mkuu wa IOM nchini Libya amesema hayo akihojiwa na Idhaa ya Umoja wa Mataifa ambapo amesema mwaka 2017 dunia ilishuhudia ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu kwa wahamiaji hasa waafrika wanaosaka hifadhi Ulaya kupitia Libya hivyo kusababisha hali ya sintofahamu kwa mustakabali wa watoto wengi wasiokuwa na walezi.
Alipoulizwa nini mpango wa IOM mwaka huu wa 2018 amesema..
(Sauti ya Othman Belbeisi)
“Tumesaini makubaliano na UNICEF ikiwa ni utekelezaji wa ushirikiano wetu katika kufuatilia kwa ukaribu zaidi na pia kutoa usaidizi unaohitajika kwa watoto wasiokuwa na wazazi au walezi, na pia kupata ufumbuzi na suluhu ya kudumu kwa watoto wahamiaji nchini Libya.”
Na vipi kuhusu wahamiaji wanaoendelea kushikiliwa magerezani nchini Libya?
(Sauti ya Othman Belbeisi)
“Tunaendelea kusaka kufungwa kwa vituo mbalimbali vinavyoshikilia wahamiaji , na kutafuta njia mbadala ya kuwahifadhi wahamiaji hao na pia kuendelea na utoaji wa misaada katika vituo mbalimbali vilivyopo nje ya mji mkuu Tripoli ili huduma muhimu ziwafikie wahitaji wote.”