Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Umoja wa Mataifa wampongeza George Weah

Rais mteule wa Liberia, George Weah (kushoto) akizungumza na mmoja wa wageni kwenye hafla iliyoandaliwa na ujumbe wa Umoja wa Mataifa nchini Liberia, UNMIL baada ya kutangazwa rasmi kwa matokeo ya duru ya pili ya uchaguzi nchini Liberia. (Picha:UNMIL Video capture)

Umoja wa Mataifa wampongeza George Weah

George Weah, ameshinda kiti cha urais nchini Liberia.

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres amemtumia salamu za pongezi na kuahidi kushirikiana naye katika kuimarisha amani na maendeleo.

Ushindi wa Bwana Weah ambaye ni mwanasoka nguli mstaafu wa kimataifa, umetangazwa leo na Tume ya Taifa ya Uchaguzi ya Liberia kufuatia duru ya pili ya uchaguzi iliyofanyika Jumanne ya wiki hii.

Bwana Guterres kupitia msemaji wake amempongeza pia makamu wa Rais wa Liberia Joseph Boakai kwa kukubali kushindwa kwenye uchaguzi huo.

Halikadhalika amepongeza wananchi wa Liberia kwa kukamilisha mchakato wa uchaguzi kwa amani, pongezi ambazo pia amezielekeza kwa waangalizi wa uchaguzi wa kitaifa, kikanda na kimataifa.

Bwana Guterres amesema hitimisho hilo la uchaguzi kwa amani ni kiashiria kuwa wananchi wa Liberia wako tayari kusonga mbele na kuendeleza amani ya kudumu, utulivu na maendeleo.

Hata hivyo amesema bado kuna changamoto na hivyo umoja ni muhimu baina ya rais mteule, serikali yake na wadau wa kisiasa.