Filamu ya Háwar yaweka bayana ukatili dhidi ya wayazidi
Filamu ya Hawar kuhusu mauaji ya kimbari dhidi ya watu wa jamii ya wayazidi Kaskazini mwa Iraq imeweka bayana ukatili waliofanyiwa watu hao. Tupate taarifa Zaidi na Flora Nducha
(TAARIFA YA FLORA)
Ikiwa imezinduliwa kwenye makao makuu ya Umoja wa Mataifa jijini New York, Marekani, Hawar ikiwa na maana kilio cha msaada imedhihirisha machungu yaliyofuatia mauaji yaliyofanywa na magaidi wa ISIL au Daesh dhidi ya wayazidi wapatao 5000 mwezi Agosti mwaka 2014.
(Sauti ya Düzen Tekkal)
“Hali ilikuwa si ya kiutu, vitendo vya kikatili walivyofanyiwa wayazidi na ISIL huwezi amini kwamba binadamu anaweza kumfanyia binadamu mwezake. Hapa tunaongelea utumwa, na vitendo visivyo vya kiutu kama ubakaji kwa wanawake na watoto, tunaongelea kufanyiwa ukatili mbele ya ndugu zako. Nikiwa ni muandaa filamu nilichukua jukumu la kupaza sauti na kuongelea janga hili kwa mataifa mbalimbali ili watu waweze kujua kwamba hii sio ukatili kwa wayazidi tu bali kwa binadamu.”
Naye Michael Blum [BLUMA] ambaye ni Mkurugezni wa shirika la kiraia nchini Ujerumani lililosaidia kuokoa zaidi ya wanawake na watoto 1000 wa kiyazidi wakati wa mauaji hayo amesema..
(Sauti ya Michael Blum)
“Wakati ISIL walipovamia vijiji vya wayazidi mwaka 2014, ujumbe wa wayazidi waishio Ujerumani ulimuendea mkuu wa mkoa wa Baden-Württemberg wakiomba msaada. Mkuu huyo akatuuliza je tufanye nini , tunajua hatuna jeshi la mkoa, basi baada ya kusoma sheria ya mkoa tukakuta kwamba kuna sheria inayoruhusu misaada ya kibinadamu. Ndipo tulipoamua kuanzisha jitihada za kuwaokoa wanawake elfu moja na kuwaleta katika mkoa Baden-Württemberg na wengine 100 katika mkoa wa mwingine.”