Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mtoto 1 kati ya 3 wanatumia inteneti, lazima walindwe:UNICEF:

Wanafunzi wakijifunza kwa kutumia tableti ya msaada uliotolewa na UNICEF katika shule ya Baigai, Kaskazini mwa Cameroon, Jumanne ya Oktoba 2017. Picha na UNICEF

Mtoto 1 kati ya 3 wanatumia inteneti, lazima walindwe:UNICEF:

Wakati fursa ya matumizi ya mtandao wa intaneti ikiongezeka ni lazima dunia hii ya kidijitali iyafanye matumizi hayo kuwa salama kwa watoto ili yaweze kunufaisha hasa wale walio katika hatari zaidi.

Hayo ni kwa mujibu wa ripoti mpya ya shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto UNICEF iliyotolewa leo ambayo inaonyesha mgawanyiko wa kidijitali unaochunguza mjadala wa sasa kuhusu athari za mtandao na vyombo vya habari vya kijamii kwa usalama na ustawi wa watoto.

UNICEF inasema licha ya uwepo mkubwa wa watoto mtandaoni huku mtumiaji 1 kati ya 3 wa intaneti duniani kote akiwa ni mtoto, ni hatua kidogo sana zilizochukuliwa kuwalinda watoto kutokana na hatari zake na kuongeza fursa yao ya kupata maudhui salama ya mtandao.

image
Wanafunzi vijana wa chuo huko Minas Gerais, Brazil. Wakiangalia video kwenye YouTube ya kampeni ya UNICEF inayotoa muongozo hususani kwa wasichana dhidi ya kuonewa na kunyanyaswa mtandaoni na jinsi gani wanaweza kujilinda. Picha na UNICEF.
Ripoti hiyo iitwayo “Hali ya watoto duniani 2017:watoto katika ulimwengu wa kidijitali” inatoa mtazamo wa kwanza kabisa wa UNICEF katika kuangalia njia tofauti za teknolojia ya kidijitali inavyoathiri watoto, fursa zao za maisha, kubaini hatari na pia fursa.

Ripoti inasema serikali na sekta binafsi hazizingatii kasi ya mabadiliko, hivyo zinawaweka watotokatika hatari mpya na kuwaharibu huku zikiwaacha nyuma mamilioni ya watoto wasiojiweza.

Anthony Lake mkurugenzi mkuu wa UNICEF amesema “kwa uzuri na ubaya, teknolojia ya kidijitali sasa ni ukweli usiogeuzwa wa maisha yetu,ulio na changamoto kuu mbili,jinsi gani ya kupunguza madhara na wakati huohuo kuongeza faida za mtandao kwa kila mtoto."

image
Watoto watatu wa familia moja huko Prince Edward Island, Canada, Desembea 12, 2016. wakiwasiliana na rafiki zao kupitia snapchat kwa kutumia simu ya mama yao. Picha na UNICEF
Hata hivyo ripoti inaonyesha mamilioni ya watoto wanakosa fursa hiyo ya mtandao, takribani theluthi ya vijana milioni 346 duniani hawako mtandaoni na Afrika ikishika mkia kwa vijana 3 ati ya 5 ukilinganisha na 1 kati ya 25 barani Ulaya, hali inayoongeza kutokuwepo usawa na kupunguza uwezo wa watoto kushiriki katika uchumi wa kidijitali.