Dola milioni 13.4 kusaidia mahitaji ya dharura Nigeria
Umoja wa Mataifa umetenga dola milioni 13.4 kwa ajili ya kusaidia watu wenye uhitaji wa haraka wa misaada wa kibinadamu nchini Nigeria
Bwana Edward Kallon ambaye ni ofisa kutoka ofisi ya kuratibu misaada ya kibinadamu ya Umoja wa Mataifa, OCHA, nchini Nigeria amesema watu milioni 8.5 wana uhitaji wa haraka wa msaada wa kibinadamu Kaskazini mashariki mwa Nigeria.
Ameyataja maeneo yaliyoathirika zaidi kuwa ni majimbo ya Borno, Adamawa na Yobe ambapo kuna maelfu ya watoto wakinamama na baba wanaohitaji msaada wa dharura.
Fedha hizo zitatumika kupambana na magonjwa ya mlipuko, matibabu ya afya, uzazi wa mpango , kukabiliana na unyanyasaji wa kijinsia na upatikanaji wa maji safi na salama kwa zaidi ya watu 125,000.