Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Zambia tumieni mikopo kuwekeza- Benki ya Dunia

Meneja wa Benki ya dunia nchini Zambia Ina-Marlene Ruthenberg. Picha: World Bank/Zambia

Zambia tumieni mikopo kuwekeza- Benki ya Dunia

Uchumi wa Zambia unaendelea kuimarika lakini ukuwaji wake bado umekuwa hafifu, hiyo ni kwa mujibu wa ripoti ya Benki ya Dunia iliyopatiwa jina ni Kwa jinsi gani Zambia inaweza kukopa bila machungu.

Ripoti hiyo inaangazia mwaka 2016 ambapo inasema kiwango cha ukuaji uchumi kilikuwa asilimia 3.6 na sasa kimeongezeka hadi asilimia  3.8 mwaka huu na matarajio ni kiwango hicho kufikia asilimia 4.7 mwaka 2019

Changamoto kubwa kwa uchumi wa Zambia kwa mujibu wa ripoti hiyo ni jinsi ya kushughulikia madeni ambapo inaelezwa kuwa kuna udhaifu.

Meneja wa Benki ya Dunia nchini Zambia Ina-Marlene Ruthenberg amesema  kuna umuhimu wa kuangalia jinsi ya kushughulikia suala la madeni ili kuhakikisha uchumi unakuwa endelevu na hela zinazokopwa zinatumika vizuri ili kuwa na ukuwaji jumuishi.

Naye mchumi mwandamizi wa benki hiyo Greygory Smith ameonya kwamba fursa ya upatikanaji wa fedha kiurahisi isiwe  sababu ya kusherehekea badala yake madeni yasimamiwe kiuangalifu na fedha hizo zitumike kuwekeza

Ripoti imeonesha kuwa pamoja na kufanya vizuri katika kuweka sera nzuri za ukopaji, kuimarisha nishati ya umeme na mavuno mazuri lakini bado nchi hiyo haijafanya vizuri kwenye sekta ya huduma, madini na ujenzi.