Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Umoja wa Mataifa watoa dola milioni 2.2 kusaidia wakazi wa Ukanda wa Gaza

Shule ya Jabalia kwenye eneo la GAza, Palestina, ambayo imeshambuliwa na makombora(maktaba). UNRWA Archives/Shareef Sarhan

Umoja wa Mataifa watoa dola milioni 2.2 kusaidia wakazi wa Ukanda wa Gaza

Umoja wa Mataifa umetoa dola milioni 2.2 kusaidia mahitaji ya dharura kwa wakazi wa Ukanda wa Gaza huko Palestina.

Mratibu wa Umoja wa Mataifa wa misaada ya kibinadamu na shughuli za maendeleo, Robert Piper amesema fedha hizo zinatoka mfuko wa kibinadamu kwa eneo la Palestina, na zinalenga huduma za afya na kuhakikisha upatikanaji wa chakula.

Bwana Piper amesema mgao huo umefanyika wkati hali inazidi kuzorota uko ukanda wa Gaza kufuatia tatizo la umeme lililoathiri watu wapatao milioni 2 kwenye eneo hilo.

Kutokana na shida ya umeme, wakazi hao wanapata huduma hiyo kwa kati ya saa nne hadi sita kwa siku na hivyo kukwamisha shughuli zao za kujipatia kipato na huduma nyingine za msingi.

Kupitia fungu hilo, mashirika ya misaada yataweza kufikisha huduma za msingi za afya huko Gaza, ikiwemo za kuboresha huduma za afya ya mama na mtoto, halikadhalika kupatia familia masikini vocha za fedha za kujinunulia mahitaji muhimu ya nyumbani.