Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ugonjwa wa kusahau kuongezeka mara 3 zaidi

Dementia, ugonjwa wa kusahau unatuathiri sote iwe kwa kuhudumia wapendwa wetu au kwa kutupata sisi wenyewePicha: WHO

Ugonjwa wa kusahau kuongezeka mara 3 zaidi

Kadri idadi ya wazee inavyoongezeka duniani, ndivyo vivyo hivyo idadi ya watu wanaougua ugonjwa wa kupoteza kumbukumbu au kusahau inaongezeka. Limesema shirika la afya duniani, WHO katika ripoti yake iliyotolewa hii leo kama anavyoelezea Leah Mushi.

(Taarifa ya Leah Mushi)

Nats..

Dementia!, ugonjwa wa kusahau unatuathiri sote iwe kwa kuhudumia wapendwa wetu au kwa kutupata sisi wenyewe!

Ndivyo inavyoanza video hii ya WHO ikizungumzia ugonjwa huo ambao hii leo imeelezwa kuwa idadi ya wagonjwa itaongezeka mara tatu ifikapo mwaka 2050.

WHO katika ripoti yake kuhusu ugonjwa huo inasema idadi itafikia milioni 152 mwaka 2050 kutoka milioni 50 hivi sasa.

Mkurugenzi  Mkuu wa WHO Dkt. Tedros Adhanom Ghebreyesus amesema takriban kila mwaka watu milioni 10 hupata ugonjwa wa kusahau, milioni 6 kati yao kutoka nchi zinazoendelea.

Amesema kwa sasa gharama za ugonjwa huo zinakadiriwa kuwa dola bilioni 818 na ifikapo mwaka 2030 gharama hizo huenda zikaongezeka na kufikia dola Trilioni 2 kiasi cha kuhofia kufifisha huduma za afya pamoja na kuongezeka kwa uhitaji wa uangalizi wa muda mrefu wa kiafya .

Hivyo amependekeza utafiti zaidi, kusaidia watoa huduma na kuondokana na unyanyapaa kwa wagonjwa.