Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mexico komesheni ubaguzi dhidi ya watu wa asili:UM

UM umeitaka serikali ya Mexico kuhakikisha inafikia uhusiano wenye usawa na heshima na watu wa asili. Picha: UM

Mexico komesheni ubaguzi dhidi ya watu wa asili:UM

Mwakilishi maalumu wa Umoja wa Mataifa kuhusu watu wa asili Tauli-Corpuz ameitaka serikali ya Mexico kuhakikisha inafikia uhusiano wenye usawa na heshima na watu wa asili ili kukomesha hali inayoendelea ya ukiukwaji wa haki za binadamu za watu wa asili.

Amesema anatambua na kupongeza hatua za kimataifa za kuiweka ajenda ya haki za watu wa asili katika jukwaa la kimataifa ikiwemo kuunga mkono kazi yake , hata hivyo amesema jukumu hilo lazima litekelezwe na serikali ya Mexicokwa kuzingatia viwango vinavyotakiwa.

Ameongeza kuwa serikali ni lazima ichukue hatua kuonyesha kwamba inazingatia haki za watu wa asili nchini humo hali ambayo itaweka mazingira yanayotakiwa kwa ajili ya mazungumzo jumuishi na endelevu na pia kutoa fursa ya kujenga Imani na uhusiano mpya baina ya jamii za watu wa asili na serikali kwa misingi ya usawa, heshima na kutokuwepo ubaguzi.

Bi Tauli-Corpuz alikuwa ziarani nchini humo tangu Novemba 8-17 ambako alikutana na watu zaidi ya 200 kutoka makundi 23 tofauti ya watu wa asili katika majimbo 18 ya Mexico na nusu yao walikuwa ni waanwake.

Miongoni mwa changamoto zinazowakabili watu wa asili nchini humo ni kutojumuishwa, kutohusishwa katika majadiliano yanayohusu haki zao ikiwemo haki ya kuishi na kutoshirikishwa katika maamuzi.