Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Hatua lazima zichukuliwe kusaka suluhu ya wakimbizi:UNHCR

Hatua lazima zichukuliwe kusaka suluhu ya wakimbizi:UNHCR

Duru ya mwisho ya majadiliano ya mkakati wa kimataifa kuhusu wakimbizi itafanyika wiki ijayo Novemba 14 na 15 mjini Geneva Uswis , kwa shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi UNHCR kutoa wito wa mapendekezo ya jinsi gani ya kushirikiana kimataifa jukumu la wakimbizi.

Majadiliano hayo yatajikita katika kupiga jeshi juhudi za kupata suluhu kwa ajili ya wakimbizi ikiwa ni pamoja na kusaidia mazingira ya hiyari na hali endelevu ya wakimbizi hao kurejea nyumbani, kuangalia njia za kupanua wigo wa fursa kwa wakimbizi kuweza kwenda katika taifa la tatu iwe ni kwa kupewa makazi, kusoma, kuungana na familia zao au kupewa vibali maalumu, lakini pia ni kuangalia jinsi gani suluhu kwa wenyeji zinaweza kusaidia wakimbizi na jamii zinazowahifadhi.

Mkutano huo pia unaangalia suala la kutokuwa na utaifa, chanzo cha wimbi kubwa la wakimbizi, na jinsi gani wadau kama sekta binafsi na taasisi za kikanda wanaweza kusaidia.

Kwa mujibu wa msemaji wa UNHCR Andrej Mahecic lengo kuu la mkutano huo ni kutoa mapendekezo halisi ya kuingizwa katika sehemu ya hatua kwa ajili ya wakimbizi, ambayo itasisitiza mfumo wa suluhu kwa wakimbizi (CRRF) na kutoa jukwaa la ushirikiano zaidi wa wajibu wenye usawa na wa kutabirika kwa ajili ya wimbi kubwa la wakimbizi.