Serikali ya Venezuela heshimu haki za binadamu – IPU
Umoja wa mabunge duniani, IPUumeeleza wasiwasi wake juu ya uamuzi wa Mahakama Kuu nchini Venezuela ya kutaka bunge la nchi hiyo liondoe kinga ya hadhi ya ubunge kwa mbunge Freddy Guevara, ambaye ni Naibu Spika wa bunge hilo.
Habari zinasema kuwa Guevara ambaye ni mwanasiasa wa upinzani na mashuhuri nchini Venezuela anatakiwa kufunguliwa mashtaka kwa uchochezi wakati wa maandamano na amesaka hifadhi kwenye ubalozi wa Chile mjini Caracas.
Katika taarifa yake, IPU imesema kwa kuwa bunge hilo ndilo chombo pekee chenye uwezo wa kisheria kufanya uamuzi huo na si mahakama, hivyo serikali ya Venezuela iheshimu katiba ya nchin na kanuni za haki za binadamu, na hasa uhuru wa kujieleza wa wabunge.
Aidha IPUimesema, itaendelea kufuatilia hali hii kwa karibu kupitia kamati yake ya haki za binadamu ya wabunge ikiwa ni njia pekee kikatiba katika kuimarisha demokrasia, na pia kuhakikisha uhuru wa taasisi ya bunge la Venezuela unatekelezwa.
Umoja huo wa mabunge duniani umesema ni matumaini yake kuwa kupitia mashauriano, pande husika zinawezak upata suluhu bora na ya kuhudumu katika janga la sasa la kibinadamu na kidemokrasia nchini humo.