Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Wadau kutoka nchi 144 wakutana Rwanda kujadili mustakabali wa rasilimali za mimea

Wadau kutoka nchi 144 wakutana Rwanda kujadili mustakabali wa rasilimali za mimea

Kikao cha 70 cha mkataba kuhusu rasilimali za mimea kwa ajili ya chakula na kilimo kimeanza leo huko Kigali nchini Rwanda kwa lengo la kufikia mwafaka wa kuimarisha ushirikiano illi kuhakikisha vizazi vijavyo vitanufaika  na lishe ya chakula na kilimo itokanayo na mimea.

Kikao hicho chini ya Shirika la kilimo na chakula duniani FAO ambacho kimekutanisha wawakilishi kutoka nchi 144 kinalenga kuimarisha ushirikiano miongoni mwa nchi ambapo wamekubaliana kutunza na kushirikiana kupata pembejeo za mimea 64 zitakazotumika kwa ajili ya utafiti na uzalishaji kwa mujibu wa mkataba wa Umoja wa Mataifa ulionza kutekelezwa mwaka 2004.

Akizungumzia kikao hicho Kent Nnadozie ambaye anaongoza bodi inayosimamia mkataba huo amesema umuhimu wa mkataba huo ni kuhakikisha usalama wa chakula kwani hakuna nchi moja ambayo inajitosheleza na hivyo ushirikiano haukwepeki.

Bwana Nnadozie amesema kufikia sasa mkataba umeleta mafanikio ikiwemo

(Sauti ya Nnadozie)

“Mkataba umefanikisha baadhi ya miradi hususan katika nchi zinazoendelea inayosaidia wakulima na wazalishaji kwa kuwasaidia kuimarisha uzalishaji wa chakula na kuweza kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi na kuendana na mabadiliko ya mazingira na mahitaji mbali mbali.”

Kauli mbiu ya kikao hicho ni Ajenda ya 2030 kwa ajili ya maendeleo endelevu na mchango wa rasilimali za mimea kwa ajili ya chakula na kilimo.