Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

SPLA yatamani kuondolewa katika orodha ya UM ya kuingiza watoto jeshini

SPLA yatamani kuondolewa katika orodha ya UM ya kuingiza watoto jeshini

Kamanda wa kikosi cha jeshi la ukombozi wa sudan SPLA huko Jonglei amesema anataka kuona ukomo wa kutumia watoto kama askari ili Sudan Kusini iweze kuondolewa kwenye orodha rasmi ya Umoja wa Mataifa ya majeshi yanayotumia watoto kama wapiganaji.

Akizungumza wakti wa warsha maalumu iliyoandaliwa na kitengo cha ulinzi wa watoto cha mpango wa Umoja wa Mataifa nchini humo UNMISS, Meja Jenerali Dau Aturjog amesema SPLAimejizatiti kuheshimu sheria za kimataifa za kibinadamu na hiyo inataka kukomesha uingizaji na utumiaji wa askati watoto katika vita.

Warsha hiyo iliyofanyika mjini Bor imehusisha askari zaidi ya 50 chini ya kauli mbiu “Watoto sio askari” kama sehemu ya kampeni iliyoanzishwa na mwakilishi maalumu wa Katibu Mkuu kwa ajili ya watoto na migogoro ya silaha, Leila Zerrougui, kwa ushirikiano na shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto UNICEF.

Lengo kuu la kampeni hiyo ni kuchagiza uungwaji mkono kwa ajili ya kuzuia na kukomesha uingizaji na utumiaji wa watoto katika vita unaofanywa na majeshi ya taifa ya usalama.