Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Guterres atoa wito kwa jamii ya kimataifa kusadia CAR

Guterres atoa wito kwa jamii ya kimataifa kusadia CAR

Akiendelea na ziara yake ya kikazi nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati CAR, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres leo amekutana na  mwenyeji wake Faustin-Archange Touadéra kuzungumzia hatma ya nchi hiyo katika  kuimarisha mshikamano na ushirikianao baina ya  jamii ya kimataifa na  nchi hiyo. Flora Nducha na taarifa kamili.

(TAARIFA YA FLORA)

Katika mazungumzo yao Guterres ameweka bayana nia ya Umoja wa mataifa na washirika wake ya  kusaidia wananchi wa jamhuri ya afrika ya kati ili kujikwamua na hali ngumu ya kiuchumi wanayokabiliana nayo,  usalama, na pia ujenzi mpya wa taifa hilo katika misingi ya amani akisisitiza

(António Guterres)

Ziara hii ni ziara ya mshikamano lakini ya ushirika na mshikamano, tuna ushirikiano wa kina na watu wa jamhuri ya Afrika ya Kati kwa sababu ya mateso , na matatizo mengi waliopitia. Lakini ujumbe muhimu wa ziara hii ni  kwa jumuiya ya kimataifa, tunahitaji kujitolea kwa kwa kiasi kikubwa, sio tu kupunguza mateso haya, lakini kwa sababu kuna fursa ya kuijenga Jamhuri ya Afrika ya Kati kwa amani, usalama na mafanikio kwa watu wake.

Aidha Bw Guterres amewaasa  wana siasa na viongozi wa dini, wakae kwenye meza ya  mazungumzo ya amani   katika kutafuta muafaka wa migogoro ya kidini na kisiasa ya wenyewe kwa wenyewe.

Katibu mkuu alitoa wito kwa jamii ya kimataifa kupitia Baraza la Usalama kuongeza misaada itakayowezesha kuongeza  nguvu kazi kwa  MINUSCA katika ufanisi wa kazi yao ya kulinda amani wa wananchi.