Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

ILO yataka makampuni ya kati na madogo kupewa mikopo

ILO yataka makampuni ya kati na madogo kupewa mikopo

Makampuni yanayotumia mikopo ya benki kama sehemu kubwa ya mitaji yao ya kazi huwa na mishahara ya juu na tija, na hupunguza gharama, lakini makampuni madogo na ya kati (SMEs) mara nyingi hayawawezi kupata au kumudu ufadhili huo, kwa mujibu wa shirika la kazi duniani  ILO.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo ya ILO iliyotolewa leo makampuni hayo ya kati na madogo yakipata mikopo kutoka benki basi riba yake inakuwa juu sana kwa kuwa yanakosa nyaraka za ukaguzi wa hesabu, historia ya malipo ya mikopo na samani ambazo zinaweza kutumika kama rehani.

Hata hivyo Deborah Greenfield naibu mkurugenzi mkuu wa ILO katika sera amesema SME’s ina jukumu muhimu sana katika kutoa ajira lakini wanakabiliwa na changamoto kubwa ya kupata fedha wanazohitaji.

Hivyo ametoa wito kwa watunga sera kwamba wanahitaji kufikiria mikakati ya kuyasaidia makampuni hayo ya kati na madogo (SME’s) kupata ufadhili huo ikiwemo mikopo ya Benki kwa ajili ya mitaji jambo ambalo linaweza kuwa na faida kubwa kwa wafanyakazi na waajiri.