Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Leo ni siku ya mwanamke wa kijijini:

Leo ni siku ya mwanamke wa kijijini:

Leo ni siku ya mwanamke wa kijijini ambayo huadhimishwa kila mwaka Oktoba 15. Katika ujumbe  maalumu kwa ajili ya siku hii mkurugenzi mtendaji wa shirika la Umoja wa Mataifa linalohusika na masuala ya wanawake UN Women Phumzile Mlambo Ngcuka amesema wanawake na wasichana ni kiungo muhimu cha maendeleo kijijini kuanzia katika familia zao n hata katika jamii, kuboresha maisha ya kijijini na ustawi kwa ujumla lakini mara nyingi jukumu na umuhimu wao huwa unasahaulika.

Na ukweli ni kwamba wanawake hao ni takribani nusu ya nguvu kazi katika mataifa yanayoendelea ikiwa ni pamoja na kuchukua sehemu kubwa ya ajira zisizo na malipo kama kutoa huduma na kazi za majumbani  katika familia.

image
Mwanamke mkulima akiwa shambani nchini Nepal:Picha na UN Women
Bi Ngcuka ameongeza kuwa uelewa na ujuzi wao katika masuala ya uhakika wa chakula na lishe, ardhi na udhibiti wa maliasili unaongeza rasilimali katika kupambana na athari za mabadiliko ya tabia nchi.

Amesema wanawake hawa wanalima sanjari na wanaume lakini hawafaidiki na mazao yao katika suala la bei, lakini pia wengi hawana fursa ya kumiliki ardhi, kupata mikopo, kuwa na sauti katika masoko na katika mfumo mzima wa chakula.

Sasa kwa pamoja UN Women, shirika la chakula na kilimo FAO, Mfuko wa kimataifa wa maendeleo ya kilimo IFAD na shirika la mpango wa chakula duniani WFP wanashirikiana kubadili hali hiyo.

Wanawake wa kijijini ni karibu robo ya watu wote duniani na wengi wa asilimia 43 ya wanawake wote ni wakulima.