Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Warsha ya kujadili imani za kishirikina na haki za binadamu yaanza Geneva

Warsha ya kujadili imani za kishirikina na haki za binadamu yaanza Geneva

Imani za kishirikina zinakwamisha haki za binadamu na ni vyema kuangazia chanzo chake ili kupata suluhu la kudumu.

Hiyo ni kauli ya Naibu Kamishna Mkuu wa haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa, Kate Gilmore aliyotoa leo huko Geneva, Uswisi wakati akifungua warsha ya siku mbili inayoangazia uhusiano kati ya imani za kishirikina na haki za binadamu.

Amesema imani hizo zimeshamiri akisema baadhi ya viongozi wa kisiasa ambao wamehusisha majanga ya kibinadamu kama vile vimbunga na hatua za serikali kupitisha ndoa za jinsia moja, na kwingineko kifo cha mtu aliyekuwa anaugua Ukimwi kikihusishwa na mtoto wa kambo.

Kama hiyo haitoshi Bi. Gilmore amesema watu wengine wanahusisha viungo vya watu wenye ulemavu wa ngozi na utajiri huku watoto wakiteswa iwapo wakiwa na ulemavu.

Naye mtoa mada Reine Alapini-Gansou ambaye ni Kamishna wa Muungano wa Afrika ametolea mfano wa nchi yake ya Benin ambako mtoto ambaye anaanza kuota jino la chini badala ya juu anaonekana kuwa ni mchawi na ananyimwa haki za msingi huku tuhuma hizo zikimzingira hadi ukubwani.

Kwa mantiki hiyo Naibu Kamishna Gilmore amesihi washiriki wa warsha hiyo ya siku mbili wakiwemo watetezi wa haki, wahanga wa vitendo vya kishirikina na wataalamu wabonge bongo ili kufahamu undani chanzo cha imani hizo kwa kuwa huleta madhara ya kimwili na kiakili.