Kuna hatua zimepigwa kukabili unyanyasaji wa kingono-Bi. Holl Lute
Kuwa na mkutano maalumu kuhusu unyanyasaji na ukatili wa kingono wakati wa mjadala wa wazi wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa ni hatua kubwa. Hiyo ni kauli ya mratibu maalum wa kuboresha mwenendo wa Umoja wa Mataifa katika kukabiliana na masuala ya unyanyasaji na ukatili wa kingono Bi Jane Holl Lute.
Akizungumza katika mahojiano na kitengo cha habari cha Umoja wa Mataifa Bi Holl Lute amesema suala la kukabiliana na ukatili wa kingono limekuwa ni moja ya vipaumbele vya Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa na kwa hivyo kujumuishwa kwa mada hiyo miongoni mwa mada zingine ni fursa muhimu katika kushirikisha viongozi, mashirika ya umma na pia kutoa ombi la kusaidia wahanga wa ukatili wa kingono.
Bi Holl Lute amesema kamati tendaji aliyoiunda, Katibu Mkuu ni hatua ya kwanza kufuatia ripoti yake iliyokuwa na sehemu nne ikiwemo kuwapa wahanga kipaumbele na mahitaji yao, kukomesha kutowajibishwa, kushirikisha wataalam na vyama vya ushirika na kuimarisha majadiliano na uwazi.
Kwa mantiki hiyo mratibu huyo maalum amesema…
(Sauti ya Holl Lute)
“Umoja wa Mataifa umekuwa katika harakati za kusaidia kwa muda mrefu wahanga wa unyanyasaji na ukatili wa kingono kwa msaada wa kimatibabu na kijamii lakini hizi ni juhudi za kuzingatia haki na heshima yao katika upande wa juhudi zetu.”
Ameongeza kuwa kufikia sasa hatua zimepigwa kwani mchakato mzima wa kushugulikia suala hilo umeimarika pia visa vya unyanyasaji vinayoripotiwa vimepungua.