WHO na wadau wahaha kudhibiti Kipindupindu Nigeria
Shirika la afya ulimwenguni, WHO na wadau wake wamechukua hatua za dharura kusaidia mamlaka nchini Nigeria kukabiliana na mlipuko wa ugonjwa wa Kipindupindu kaskazini-mashariki mwa nchi hiyo.
Hadi sasa wagonjwa 69 wameripotiwa huku watano kati yao wamefariki dunia kwenye kambi ya Muna Garage iliyoko kwenye viunga vya mji mkuu wa jimbo la Borno, Maiduguri.
Katika eneo hilo kuna wakimbizi zaidi ya 44,000 ambao wamekimbia ghasia na njaa.
WHO inasema hivi sasa inahaha kutambua wagonjwa kama njia moja ya kudhibiti kuenea kwa kasi kwa ugonjwa huo hasa kwenye maeneo ambako huduma za majisafi na salama ni adimu.
Tayari vituo vya matibabu vimeanzishwa sambamba na kampeni ya chanjo dhidi ya ugonjwa huo.