Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Baadhi ya nchi zaitikia wito wa kusaidia Sierra Leone

Baadhi ya nchi zaitikia wito wa kusaidia Sierra Leone

Leo ni siku ya tano tangu Sierra Leone ikumbwe na maporomoko ya udongo na mafuriko kutokana na mvua zinazoendelea kunyesha nchini humo ambapo bado usaidizi wa kimataifa unatakiwa ili kuendelea kusaka mamia ya watu ambao bado hawajulikani walipo na pia kusaidia walioathiriwa na janga hilo.

Umoja wa Mataifa unasema watu zaidi ya 400 wamefariki dunia na harakati z a uokozi zinaendelea huku baadhi ya nchi zikielekeza usaidizi wao kwa Sierra Leone.

Jens Laerke msemaji wa ofisi ya Umoja wa Mataifa ya inayohusika na usaidizi wa kibinadamu OCHA amesema

(Sauti ya Jens)

“China imesema itatoa dola milioni Moja, Muungano wa Ulaya umetoa ahadi ya awali ya Euro Laki tatu kwa familia zilizoathirika, Ireland, Uingereza, Guinea, Nigeria na Liberia wote wametoa ahadi mbali mbali, halikadhalika Ubelgiji na Uswisi.”

Halikadhalika amesema kufuatia ombi la serikali siku mbili zilizopita, OCHA imeunda jopo la watu Saba ambalo litasaidiana na serikali na taasisi za kimataifa kutathmini mahitaji ya muda mfupi, kati na mrefu kwa wahanga wa tukio hilo.