Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

ILO kutangaza jopo la mustakabali wa ajira

ILO kutangaza jopo la mustakabali wa ajira

Shirika la kazi ulimwenguni ILO, linatarajia kuanzisha tume ya ngazi ya juu ya kimataifa, tume itakayojumuisha wataalamu 20 ambao pamoja na mambo mengine wataangalia namna mabadiliko ya kazi yanavyoweza kukidhi viwango vya sheria.

Katika taarifa yake hii leo, ILO imesema majina ya wanachama wa tume hiyo maaluma kwa ajili ya mustakabali wa kazi, yatatangazwa mnamo Agosti 21 mjini Geneva Uswisi, ikiwa ni juhudi za ILO katika mikakati ya mustakabali wa kazi zilizoasisiwa na shirika hilo mwaka 2013.

Wataalamu katika tume hiyo watatandaa ripoti huru ambayo itawasilishwa kwenye mkutano wa maadhimisho ya miaka 100 tangu kuanzishwa ILO mwaka 2019, imesema taarifa hiyo.

Shirika hilo la kazi ulimwenguni limesema miongoni mwa watakaoshuhudia kutangazwa kwa tume hiyo ni pamoja na Wenyeviti wenza wa tume hiyo Rais wa Mauritius Ameenah Gurib-Fakim na Waziri Mkuu wa Sweden Stefan Löfven.