Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Jumuiya ya kimataifa lazima ihakikishe hakuna mtu wa LDC’s anayesalia nyuma:

Jumuiya ya kimataifa lazima ihakikishe hakuna mtu wa LDC’s anayesalia nyuma:

Watu kutoka mataifa yenye maendeleo duni au LDC’s wengi hawajiwezi , masikini na wako katika hatari ya kuachwa nyuma na treni ya utekelezaji wa malengo ya maendeleo endelevu au SDG’s ifikapo mwaka 2030.

Akizungumza na waandishi wa habari kwenye makao makuu ya Umoja wa Mataifa hapa New york Marekani leo, kuhusu uzinduzi wa ripoti yenye kichwa "Hali ya nchi zenye maendeleo duni (LDC’s) 2017” Fekitamoeloa Katoa 'Utoikamanu, msaidizi wa Katibu Mkuu na mwakilishi mkuu wa ofisi ya Umoja wa Mataifa inayowakilisha nchi zenye maendeleo duni, nchi zinazoendelea zisizo na bahari na mataifa yanayoendelea ya visiwa vidogo (UN-OHRLLS) amesema..

(SAUTI FEKITAMOELOA)

“LDC’s zinasalia kuwa ndio nchi zisizojiweza duniani, huku idadi kubwa ya watu wake wakiishi kwenye umasikini uliokithiri, wakiwa na matumaini kidogo sana ya kuboresha hali yao.ili kuhakikisha hakuna anayesalia nyuma , jumuiya ya kimataifa inatakiwa kuliangalia kwa makini kundi la nchi hizi”.

Amesema ikiwa imesalia miaka mitatu ya ukomo wa utekelezaji wa mpango kazi wa Instanbul kwa ajili ya LDC’s hapo 2020, bado wanasuasua katika mambo muhimu kama vile ukuaji wa pato la kitaifa bado uko chini, wakati umasikini umepungua katika baadhi ya nchi za LDC’s lakini bado haujatokomezwa, idadi ya watu walio na fursa ya kupata nishati ya umeme bado iko chini kwa viwango vya mpango wa Instabul na pia SDG’s na pia idadi ya watu wanaotumia teknolojia ya internet ingawa imeongezeka lakini kasi yake bado ni ndogo kwa nchi hizi. Hivyo amesisitiza hatua zinahitajika sasa hasa za uwekezaji katika nchi za LDC’s.

Naye Masud Bin Momen, Mwakilishi wa Kudumu wa Bangladesh kwenye Umoja wa Mataifa na mwenyekiti wa nchi zenye maendeleo duni (LDC’s) amesisitiza..

(SAUTI MASUD MOMEN)

“Kumekuwa na hatua za kufikia ajenda ya 2030 kote duniani lakini hatua hiyo haitoshelezi na hailingani miongoni mwa nchi. Kutokuwepo usawa na pengo la kidijitali baina ya nchi za LDC’s na zingine duniani limeongezeka na athari za majanga na adha zingine zimefanya matarajio ya maendeleo katika nchi hizo kuwa katika hatari kubwa..”