Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Adama Dieng ziarani DRC kuangalia hali halisi Kasai

Adama Dieng ziarani DRC kuangalia hali halisi Kasai

Mshauri maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa kuhusu mauaji ya halaiki Adama Dieng yuko ziarani nchini Jamhuri ya kidemokrasia ya Congo, DRC kuangazia hali ilivyo kwenye majimbo yaliyoko eneo la Kasai.

Ziara hiyo ya siku sita inakuja wakati kumeripotiwa ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu ikiwemo mauaji ya hata raia wasio na hatia.

Naibu msemaji wa ujumbe wa Umoja wa Mataifa nchini humo, MONUSCO Théophane Kinda amesema Bwana Dieng anaangalia hatua zinazoweza kuchukuliwa ili kuepusha mauaji zaidi.

Tayari ameshakutana na viongozi wa mamlaka ya serikali, dini na vikundi vya kiraia huko Kinshasa, Kananga na Tshikapa na mwishoni mwa ziara yake tarehe 25 mwezi huu atakuwa na mkutano na waandishi wa habari.