Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mafuriko Sri Lanka, IOM yatuma timu kutathmini

Mafuriko Sri Lanka, IOM yatuma timu kutathmini

Shirika la uhamiaji la Umoja wa Mataifa, IOM limepeleka timu tatu za kutathmini haraka madhara ya mafuriko na maporomoko ya udongo nchini Sri Lanka ambapo hadi sasa watu 177 wamefariki dunia.

IOM inasema watu 109 hawajulikani walipo ambapo timu hiyo inakwenda katika wilaya nne zilizoathirika zaidi ambazo ni Ratnapura, Galle, Matara na Kalutara, zilizoko kusini mwa nchi hiyo.

Pamoja na vifo, IOM inasema pepo hizo za Monsoon zimesambaratisha kabisa nyumba 768 na sasa watu 361 wamesaka hifadhi katika makazi ya muda.

Mafuriko ya sasa yaelezwa kuwa mabaya zaidi kuliko ya mwezi Mei mwaka 2003 ambapo nyumba 1,000 ziliharibiwa huku watu 250 wakifariki dunia.