Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Keating akaribisha kuapishwa kwa Rais wa Galmudug Somalia

Keating akaribisha kuapishwa kwa Rais wa Galmudug Somalia

Mwakilishi maalumu wa Umoja wa Mataifa nchini Somalia, Michael Keating, amekaribisha kuapishwa kwa Ahmed Ducaale Geelle “Xaaf” kama Rais wa Galmudug katika hafla iliyofanyika leo Jumanne mjini Adaado.

Akihutubia katika hafla hiyo Keating amempongeza Rais Xaaf na kusema amepatiwa jukumu kubwa la kuhakikisha anatoa uongozi bora kwa watu wa Galmudug ikiwemo kuwapa fursa za ajira na kukuza uchumi, miundombinu , huduma za jamii, ulinzi na kuboresha taasisi za serikali.

Ameongeza kuwa jumuiya ya kimataifa iko tayari kuisaidia Galmudug, ikiwa ni pamoja na utekelezaji wa mkakati wa kitaifa wa usalama, lakini maridhiano ndio hatua ya kwanza muhimu ya kuhakikisha utulivu jimboni humo.

Keating amesisitiza kwamba ili kuwa na serikali jumuishi majadiliano ni lazima yaanze sasa huku akitoa wito kwa Rais huyo kuhakikisha mgogoro wa Galkacyo, unatatuliwa.