Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ongezeko la vurugu CAR lawafungisha virago watu 88,000:UNHCR

Ongezeko la vurugu CAR lawafungisha virago watu 88,000:UNHCR

Fedha zaidi zahitajika haraka ili kuwasaidia watu zaidi ya 88,000 waliolazimika kukimbia ongezeko la machafuko nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati CAR.

Kwa mujibu wa shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi UNHCR, tangu kuzuka upya kwa machafuko miongoni mwa waasi mwezi May watu 68,000 wamezihama nyumba zao na kuwa wakimbizi wa ndani huku wengine elfu 20 wameenda kusaka hifadhi ya ukimbizi nchini jirani ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo DRC. Babar Baloch ni msemaji wa UNHCR Geneva

(SAUTI YA BALOCH)

“Ili kusaidia watu ambao wametawanywa hivi karibuni , UNHCR inatoa wito wa msaada wa haraka katika ombi lake la ufadhili wa dola milioni 209.2 kwa ajili ya hali ya CAR ombi ambalo hadi sasa limefadhiliwa asilimia 6 tu.”

Ameongeza kuwa shughuli za waasi katika miji iliyo mpakani na DRC pamoja na taarifa za uwezekano wa mashambulizi vimewafanya watu kufungasha virago katika maeneo ya Haute Kotto na Mbomou nchini CAR ambapo katika wiki mbili zilizopita pekee watu zaidi ya elfu 20 wamekimbia.