Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Watoto 150 wafariki kila siku Myanmar: UNICEF

Watoto 150 wafariki kila siku Myanmar: UNICEF

Takriban watoto 150 wenye umri wa chini ya miaka mitano nchini Myanmar wanafariki dunia kila siku, na asilimia 30 wanakumbwa na utapiamlo uliokithiri, wengi wao kutoka mashinani, imesema ripoti ya Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Watoto, UNICEF leo.

Utafiti huu unaonyesha ukosefu wa usawa katika juhudi zinazofanywa na serikali katika mageuzi na maridhiano baada ya mgogoro wa muda mrefu.

Kwa mujibu wa utafiti huo, karibu maisha ya watoto milioni 2.2 hawana uhakika wa amani huku wakikabiliwa na kiwango kikubwa cha umasikini na ukosefu wa fursa na hofu ya machafuko inayoendelea.

Shirika hilo la kuhudumia watoto limeongeza licha ya mafanikio kadhaa ya kiuchumi na kijamii kutokana na juhudi za serikali, bado watoto waliko vijijini nchini Myanmar wanahaha kusaka maisha bora.