Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Wito wa kuchunguza vifo vya waandamanaji Venezuela wakaribishwa-UM

Wito wa kuchunguza vifo vya waandamanaji Venezuela wakaribishwa-UM

Nchini Venezuela hali ya vifo katika maandamano ya kupinga serikali inasikitisha imesema ofisi ya haki za binadamu ya Umoja wa Mataifa Ijumaa.

Hadi vifo 42 vimethibitishwa ambavyo vinahusiana na maandamano ya karibuni dhidi ya Rais Nicolas Maduro, yaliyochagizwa na kuongezeka kwa hofu na hali ngumu ya kiuchumi.

Ofisi ya haki za binadamu ya Umoja wa mataifa ambayo inajaribu kupata fursa kuingia nchini humo imesema inakaribisha tangazo la mwanasheria mkuu wa nchini hiyo kwamba uchunguzi utafanyika dhidi ya vifo vya waandamanaji. Rupert Colville ni msemaji wa ofisi ya haki za binadamu Geneva.

(RUPERT COLLIVELE)

“Bila shaka kuna shutuma za matumizi ya nguvu kupita kiasi yaliyofanywa na vikosi vya usalama, hivyo nasisitiza tena umuhimu wa kutekeleza wajibu kwa kuzingatia viwango vya kimataifa vya haki za binadamu. Pia kuna ripoti za ghasia za makundi yenye silaha . Tunawachagiza waandamanaji kutumia njia za amani , nadhani hilo ni la muhimu sana , inasikitisha na kutia hofu kinachoendelea Venezuela.”

Bwana Colville pia ameelezea wasiwasi wake kuhusu raia kukamatwa na kupelekwa kwenye mahakama za kijeshi.