Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Tahadhari ya mapema ya majanga, itaokoa maisha na kupunguza hasara-WMO

Tahadhari ya mapema ya majanga, itaokoa maisha na kupunguza hasara-WMO

Mabadiliko ya tabianchi yanayohusiana na mabadiliko ya kimaeneo na hali mbaya ya hewa inamaanisha mamilioni ya watu wako katika hatari ya kukumbwa na majanga kama mafuriko, joto la kupindukia na hatari zingine limesema shirika la kimataifa la utabiri wa hali ya hewa WMO.

Limeongeza kuwa uimarishaji wa mifumo ya kutoa tahadhari ya mapema na uratibu mzuri wa kupunguza hatari ya majanga sasa ni muhimu kuliko wakati mwingine wowote.

Na ili kukabiliana na changamoto hizo mkutano wa kimataifa utakaofanyika wiki ijayo Cancun Mexico utazindua mkakati wa pamoja wa kuboresha mifumo ya kutoa tahadhari kwa ajili ya majanga mbalimbali na kuchukua hatua zinazostahili kwani zaidi ya asilimia 80 ya majanga ya asili duniani yanasababishwa na hali ya hewa au maji.

Mkutano huo “Tahadhari ya mapema ya majanga mbalimbali:okoa maisha, punguza hasara” utakaoanza Mei 22-23 umeandaliwa na WMO, ofisi ya Umoja wa Mataifa ya upunguzaji hatari ya majanga UNISDR kwa ushirikiano na wadau wengine mbalimbali wa kimataifa ikiwemo Benki ya Dunia.