Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Watoto na barubaru wenye jinsia mbili au waliobadili wasitengwe #IDAHOT

Watoto na barubaru wenye jinsia mbili au waliobadili wasitengwe #IDAHOT

Watoto na barubaru wenye jinsia mbili, waliobadili jinsia au wanaojihusisha na ushoga wanapaswa kulindwa dhidi ya ubaguzi, kutengwa, ghasia na unyanyapaa.

Hiyo ni kwa mujubi wa kundi la wataalamu wa haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa katika kuadhimisha hii leo siku ya kimataifa dhidi ya chuki ya wapenzi wa jinsia moja, waliobadili jinsia na wale wenye jinsia mbili.

Wamesema katika zama za sasa, watoto na barubaru wengi kwenye kundi hilo wanakumbwa na ubaguzi, mateso na kutengwa na familia zao na hivyo kuwa hatarini kukumbwa na ukatili shuleni, kazini na hata ndani ya familia zao kwa kigezo cha kutakasa familia.

Kwa mantiki hiyo wametoa wito kwa serikali kuwa na sera na kanuni zitakazohakikisha wanapata haki zao za msingi za kuendelezwa ili waweze kuwa huru kutoa mawazo yao na hatimaye kufikia ustawi wao.

Mathalani haki ya afya, elimu wakisema kuwa iwapo ushoga unaharamishwa, watoto au barubaru wa aina hiyo hawatakuwa huru kusaka huduma za afya na hivyo wanaweza kufariki dunia kwa magonjwa yanayoweza kuepukika.