Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Kongamano la China ni fursa ya kilimo na SDGs-FAO

Kongamano la China ni fursa ya kilimo na SDGs-FAO

Akiwa mjini Beijing China, Mkurugenzi Mkuu wa shirika la kilimo na chakula FAO José Graziano da Silva amesema kongamano la kimataifa kuhusu mradi wa China uitwao ukanda mmoja barabara moja, ni fursa ya kukuza kilimo na kufanikisha maendeleo endelevu SDGs.

Amesema kilimo ni sekta muhimu kwani inajumisha asilimia 25 ya pato la ndani na zaidi ya asilimia 40 ya ajira katika nchi nyingi duniani.

Katika hotuba yake Bwana da Silva amesisitiza kuwa kilimo huwezesha ajira na ustawi wa mamilioni ya wakulima na wafugaji na kuongeza kuwa kilimo huwezesha uhakika wa chakula na lishe duniani.

Kongamano hilo lililomalizika hii leo mjini Beijing China, limewaleta pamoja viongozi wa nchi 29, likilenga katika kukuza biashara kati ya bara Asia, Afrika, Amerika Kusini na Ulaya.