Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Tatueni mtafaruku wa nishati Gaza-Mladenov

Tatueni mtafaruku wa nishati Gaza-Mladenov

Afisa wa ngazi ya juu wa Umoja wa mataifa ametoa wito wa kutatua mtafaruku wa umeme Gaza ambako mtambo pekee wa nishati hiyo umeishiwa mafuta.

Bwana Nikolay Mladenov ambaye ni mratibu maalumu wa Umoja wa mataifa kwa ajili ya mchakato wa amani wa Mashariki ya Kati amesema athari za kijamii, kiuchumi na kisiasa za tatizo hilo la umeme zisichukuliwe kimzaha.

Katika taarifa yake iliyotolewa Jumatano Mladenov amesema Wapalestina walio Gaza ambao wanaishi katika mgogoro wa muda mrefu wa kibinadamu hawawezi kuendelea kuwekwa mateka na kutokubaliana, mgawanyiko na kufungwa kwa njia.

Ametoa wito kwa pande zote ikiwemo jumuiya ya kimataifa kuja pamoja na kutafuta suluhu ya zahma hii. Bwana Mladenov amesema kufanyia mabadiliko kampuni ya umeme Gaza ni muhimu katika kuboresha mapato na kuwa wazi kwa mujibu wa viwango vya kimataifa na wakati huohuo jumuiya ya kimataifa ni lazima itoe ufadhili na kusaidia mchakato huo. Nayo Israel ameongeza ni lazima isaidie kwa kuruhusu uingizaji wa vifaa vya ukarabati wa mtambo huo wa umeme.