Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ufadhili wa Marekani wasaidia kupambana na utapiamlo Msumbiji

Ufadhili wa Marekani wasaidia kupambana na utapiamlo Msumbiji

Mchango uliotolewa na serikali ya Marekani utaliwezesha shirika la mpango wa chakula duniani WFP kuwasaidia wanawake wajawazito, kina mama wanaonyonyesha na watu wanaoishi na virusi vya ukimwi (VVU) au wenye kifua kikuu nchini Msumbiji.

Dola milioni 2.7 za ufadhili wa ziada zilizotangazwa Jumatano zitatumika kutoa chakula mchanganyiko kitakachosaidia kutibu utapia mlo miongoni mwa watu wa makundi hayo ,zikilenga kuwafikia watu 21,000 katika majimbo matano yaliyoathirika zaidi na ukame.

WFP inasema watu wanaoishi na VVU au kifua kikuu ndio waathirika wakubwa wa tatizo la uhakika wa chakula na utapia mlo, lakini pia dawa wanazokunywa bila lishe bora haziwezi kufanya kazi ipasavyo.