Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

UNICEF na wadau wasaidia zaidi ya 145,000 kwenye baa la njaa Sudan kusini:

UNICEF na wadau wasaidia zaidi ya 145,000 kwenye baa la njaa Sudan kusini:

Mwezi mmoja tangu kutangazwa kwa baa la njaa katika baadhi ya sehemu nchini Sudan kusini , shirika la Umoja wa mataifa la kuhudumia watoto UNICEF, kwa pamoja na lile la mpango wa chakula WFP na washirika wengine wamefikisha msaada wa kuokoa maisha kwa watu 145,000 wakiwemo watoto 33,000 wa chini ya umri wa miaka mitano.

Timu ya dharura ya watu 13 imepelekwa jimbo la Unity ambako zaidi ya watu 10,000 wanaishi katika kata mbili zilizokumbwa na baa la njaa.

Kwa mujibu wa kaimu mwakilishi wa UNICEF Sudan Kusini Jeremy Hopkins, kukiwa na zaidi ya robo milioni ya watoto wanaokadiriwa kuwa katika utapia mlo uliokithiri hatua za haraka zinahitajika kuwanusuru. Na kupitia mpango huo wa timu ya dharura UNICEF imeweza kuwapima watoto zaidi ya elfu tano mia saba wa chini ya miaka mitano na kuwachanja zaidi ya 25,000 dhidi ya polio na surua.