Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Sasa tuna uwezo wa kutuma haraka kikosi imara- Ladsous

Sasa tuna uwezo wa kutuma haraka kikosi imara- Ladsous

Mkutano wa viongozi uliofanyika miaka miwili iliyopita kuhusu ulinzi wa amani uliboresha operesheni za ulinzi wa amani za Umoja wa Mataifa.

Hervé Ladsous, mkuu wa operesheni za ulinzi wa amani za Umoja wa Mataifa amesema hayo akihojiwa na Idhaa ya umoja huo, wakati huu ambapo anamaliza muda wake hii leo tarehe 31 mwezi Machi.

Amesema mkutano huo ulipitisha hatua ambazo kwazo hivi sasa zimeimarisha ulinzi wa amani, mathalani..

 (Sauti ya Ladsous)

“Tumekuwa na uwezo wa kupeleka kikosi tangulizi ndani ya siku 30 hadi 60 jambo ambalo lingalikuwa haliwezekani miaka miwili iliyopita.”

Hata hivyo amesema changamoto iliyosalia ni uwezeshaji wa vifaa kwa baadhi ya vikosi lakini suala hilo linashughulikiwa kwa kupitia mazungumzo na wawezeshaji.

Bwana Ladsous amesema ingawa idara hiyo ya operesheni ya ulinzi wa amani imekuwa ikipunguza gharama bado haikupunguza ubora wa huduma au vifaa vinavyotakiwa.