Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Hali ya kibinadamu yazidi kuzorota Somalia-UM

Hali ya kibinadamu yazidi kuzorota Somalia-UM

Wakati tishio la baa la njaa likizidi kunyemelea Somalia, hali ya kibinadamu inaendelea kuzorota nchini humo, umesema Umoja wa mataifa Jumatano. Takribani watu 257,000 wametawanywa nchini Somalia tangu Novemba 2016 hadi Februari mwaka huu, huku wengine zaidi ya elfu nne wakivuka mpaka kuingia Ethiopia .

Ombi la msaada halijafikia hata nusu na gonjwa la kipindupindu na kuhara vikizidi kutishia maisha ya maelfu kama anavyofafanua msemaji wa Umoja wa Mataifa Farhan Haq akitoa taarifa kwa waandishi wa habari mjini New York

(Sauti ya Farhan)

“Visa zaidi ya elfu 13 vya kuhara na kipindupindu vinashukiwa na vifo zaidi ya 300 vimeripotiwa tangu mwanzoni mwa mwaka. Na kwa ujumla ombi la msaada wa kibinadamu kwa Somalia mwaka 2017 la dola milioni 864, hadi sasa ni asilimia 31 tu iliyofadhiliwa.”

Ameongeza kuwa ombi hilo linatarajiwa kufanyiwa tathimini hivi karibuni kwa kuzingatia ongezeko la mahitaji ya watu kutokana na tishio la baa la njaa.