Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mkutano wa IAEA Sudan kusaidia ufadhili wa saratani

Mkutano wa IAEA Sudan kusaidia ufadhili wa saratani

Mkutano ulioandaliwa kwa ushirikiano na shirika la kimataifa la nguvu za atomic IAEA kusaidia ufadhili wa miradi ya kukabiliana na saratani katika nchi zilizolemewa na ongezeko la maradhi hayo umemalizika leo Jumatano nchini Sudan.

Mkutano huo wa siku mbili uliofanyika mjini Khartoum umetathimini mapendekezo ya kutoa huduma ya saratani kwa wakimbizi na kuongeza ufadhili kwa ajili ya kupambana na saratani ya shingo ya kizazi inayokatili maisha ya wanawake wengi duniani.

Mkutano huo umetokana na juhudi zilizozinduliwa mwaka 2012 na IAEA , shirika la jumuia ya nchi za Kiislam OIC, na benki ya Kiislam ya maendeleo, ili kuchagiza rasilimali na msaada wa mafunzo kama sehemu ya kudhibiti saratani katika nchi ambazo ni wanachama wa mashirika yote hayo matatu, ambayo pia yalitia saini mkataba mwaka 2016 wa kusaidia ushirika wao.

Mkutano huo umewaleta pamoja wawakilishi kutoka sekta ya afya na mawaziri wa fedha kutoka mataifa 16 yaliyowakilisha mapendekezo zikiwemo nchi 12 za Afrika.